|
Wafanyabiashara wa Msasani wakarabati soko kwa Mil. 25/-
2009-05-05 20:49:22
Na Abdul Mitumba, Kinondoni
Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni ikishirikiana na wafanyabiashara wa soko la barabara ya Maandazi pale Msasani, imetumia zaidi ya shilingi milioni 25.5 kwa ajili ya kulikarabati soko hilo.
Katika fedha zote, wafanyabiashara hao walichangia shilingi milioni 15 na manispaa ikachangia bati 700, ambazo zimetumika kujenga upya paa za soko hilo lililogawanywa katika sehemu kuu nne.
Sehemu hizo ni pamoja na za wauza samaki na kuku, nafaka, matunda na mbogamboga na pia sehemu ya mama lishe.
Mwenyekiti wa wafanyabiashara sokoni hapo, Bw. Ali Hemedi, amesema kuwa fedha hizo zimewezesha soko kuwa katika hali bora inayotoa fursa kwa wafanyabiashara kuendesha shughuli zao kwa ufanisi.
``Kabla ya ujenzi huu, mabanda ya soko yalikuwa duni. Watu walishindwa hata kuinuka wakati wakiondoa uchafu,`` anasema Hemedi.
Hata hivyo, Hemedi amelazimika kuhimiza suala la usafi wa soko ili kuliweka katika hali ya usafi wakati wote, hasa wakati huu wa mvua.
Hemedi alikuwa akizungumza mbele ya Ofisa Mtendaji wa Kata ya Msasani, Bw. Gilbert Mushi aliyetembelea soko hilo ili kujionea shughuli zinazoendelea sokoni hapo na kusikiliza kero zao, ambazo ni pamoja na zile za uchafu.
|