|
Akamatwa na vifaa vya kutengenezea noti bandia
2009-05-08 13:44:40
Na Luppy Kung`alo
Polisi mkoani Shinyanga, inamshikilia Marko Sayi (26), mkazi wa Nyahanga wilayani Kahama baada ya kumkamata akiwa na vifaa mbalimbali vya kutengenezea noti bandia.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Shaibu Ibrahim, alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa akiwa na zana hizo kwenye nyumba ya kulala wageni ya Nkoba iliyopo Mji Mdogo wa Maganzo wilayani Kishapu.
Ibrahim alitaja vifaa hivyo kuwa ni karatasi zilizokatwa ili kutengenezea fedha bandia, wino, pamba na fedha halali za noti zenye thamani ya sh10,000 kila moja.
``Nashukuru raia wema walioweza kutupa taarifa za mtuhumiwa huyo ambazo nasi bila kusita tulizifanyia kazi na kufanikiwa kumnasa saa 6:00 usiku akijiandaa kutengeneza fedha hizo,`` alisema Ibrahim.
Alisema uchunguzi wa awali umebaini Sayi, alikuwa tayari ametengeneza fedha bandia zenya thamani ya sh. milioni tano.
Aliongeza kuwa sh. milioni 2.5 ambazo ni bandia alikuwa amewapa watu mbalimbali ambao hawajafahamika ili wazitumie kununulia mazao na mifugo toka kwa wananchi.
Kamanda huyo alitoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na polisi na wawe makini kuchunguza nyendo za watu wanaowatilia wasiwasi.
|