|
Wivu wa mapenzi waua mke Mara
2009-05-08 13:47:15
Na Willibroad Tungaraza, Serengeti
Mkazi wa Kijiji cha Magange Kata ya Ring`wani, wilayani Serengeti, Mkoa wa Mara, Rose Sagati (24), amefariki dunia baada ya kuvunjwa shingo na mme wake Sagati Mwita, ambaye ni mganga wa kienyeji kwa wivu wa mapenzi.
Tukio hilo lilitokea usiku wa Aprili 27 mwaka huu katika kijiji hicho kisha mtuhumiwa kukimbilia kusikojulikana.
Diwani wa Kata hiyo, Laurian Kyariga, alisema kwamba siku ya tukio mtuhumiwa alikuwa amekwenda kijiji cha Maburi ndipo mke wake akampigia simu kumuulizia kama atarejea nyumbani.
``Hata hivyo wakati mumewe anarejea nyumbani alimdanganya mke wake kwamba hatarejea hivyo marehemu akaondoka usiku huo na wanaume wengine na kukutana njiani na mme wake,``alisema Diwani.
Kyariga alisema kwamba baada ya kukutana na mkewe njiani usiku akibebwa na wanaume kwenye baiskeli, wanaume walikimbia.
Alisema mwanamume alimchukua mkewe hadi nyumbani ambapo alimpa kipigo.
Polisi wilayani hapa wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa marehemu ambaye alikuwa mjamzito alifariki baada ya kunyongwa shingo.
Wagonjwa waliokuwa wanapatiwa matibabu walikimbia baada ya kuripoti tukio hilo kwa Mwenyekiti wa Kitongoji ambaye naye alitoa taarifa Polisi. Mtuhumiwa anaendelea kusakwa baada ya kutoweka.
|